Kwa mujibu wa ripota wa Shirika la Habari la Hawza, Ayatollah A‘rafi, mkuu wa hawza nchini Iran, katika mkutano mkuu wa wasimamizi wa taasisi za hawza uliofanyika katika Kituo cha Usimamizi wa Hawza za Wanawake, aliwapongeza wananchi kwa kuleta hamasa kubwa katika matembezi ya tarehe 22 Bahman na siku za mwisho za mwezi wa Sha‘ban, na kusisitiza umuhimu wa maandalizi ya pande zote ya hawza za elimu ya dini kwa ajili ya kuingia katika mwezi mtukufu wa Ramadhani, akiuita mwezi huo kuwa “chuo kinachounga mkono dini na tablighi”.
Mkuu wa hawza akirejelea sunna ya Mtume Mtukufu (s.a.w.w.) na Maimamu watoharifu (a.s.) ya kutoa tahadhari na kuamsha watu kujiandaa kwa ajili ya mwezi wa Ramadhani, alisema: Katika vyanzo vya riwaya, kuna zaidi ya majina na sifa mia moja za mwezi mtukufu wa Ramadhani, na hakuna kipindi kingine cha wakati kilichopewa maelezo mapana kiasi hicho.
Mjumbe wa Baraza Kuu la Hawza, huku akibainisha kuwa Ramadhani ni “chombo chenye nuru cha kudhihiri majina na sifa za Mwenyezi Mungu”, aliongeza: Moja ya sifa za ajabu za mwezi huu ni kuongezeka kwa thamani ya matendo; kiasi kwamba kwa mujibu wa riwaya, kusoma aya moja ya Qur’ani ndani ya Ramadhani ni sawa na kuhitimisha Qur’ani nje ya Ramadhani, na baadhi ya matendo hupata thamani hadi “mara milioni”.
Aliendelea kusema: Katika mwezi huu, hata matendo ya halali ya mtu anayejilinda kwa heshima ya Ramadhani hupata rangi ya ibada; mbali na hilo, kufutwa na kusamehewa madhambi kunajitokeza kwa namna ya pekee, kiasi kwamba mtu, kwa kuzingatia masharti, hutoka katika mwezi huu akiwa msafi kama siku aliyozaliwa.
Ayatollah A‘rafi alisisitiza kuwa maandalizi ya Ramadhani hawza si ya mtu mmoja mmoja tu, akasema: Maandalizi haya yanapaswa kutekelezwa katika ngazi ya taasisi, kiutawala na kimkakati, na taasisi za hawza zinaweza kubadilisha hali ya kiroho ya jamii katika mwezi huu.
Umoja wa taasisi za hawza; uzoefu uliofanikiwa katika utumaji wa wahubiri
Akishukuru ushirikiano wa taasisi za hawza katika mipango ya pamoja, alirejelea uzoefu wa karibuni wa uratibu mpana katika utumaji wa wahubiri na kusema: Katika suala la utumaji mpana wa wahubiri, taasisi zote zilisimama pamoja na kuchukua hatua kwa umoja na mshikamano; umoja huu pia ulipata pongezi kutoka kwa Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi.
Mkuu wa hauza za elimu ya dini aliuita mshikamano huu wa kiutawala “neema ya Mwenyezi Mungu” na kusisitiza umuhimu wa kuuimarisha katika ngazi za mikoa.
Kutambua mapambano ya ustaarabu wa Magharibi; jukumu la msingi la hawza
Ayatollah A‘rafi, huku akirejelea “mapambano makubwa ya ustaarabu” kati ya Mapinduzi ya Kiislamu na ustaarabu wa kisasa wa Magharibi, alisema: Wanazuoni wa dini wamesimama mstari wa mbele katika “mapambano makubwa ya ustaarabu dhidi ya Magharibi”, na kuutambua uwanja huu ni dharura ya kimkakati; bila kuelewa nafasi yetu katika vita hii ya kielimu na ya ustaarabu, harakati zetu zitakuwa pungufu.
Aliongeza kuwa; Mapinduzi ya Kiislamu ni harakati ya kwanza ya kisasa iliyoingia katika uwanja huu kwa mtazamo wa kushambulia kiitikadi, na akasema: Chanzo cha mashinikizo dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu si uwezo wa kijeshi pekee, bali ni makabiliano ya kimawazo na kiitikadi.
Mkuu wa hawza za elimu ya dini alisisitiza: Tukifaulu kuwasilisha ipasavyo mazungumzo na fikra zetu, tutakuwa na hadhira kubwa duniani, na uzoefu wa shughuli za kimataifa umeonesha ukweli huu.
Misingi ya ustaarabu wa Magharibi
Ayatollah A‘rafi, akifafanua misingi ya ustaarabu wa Magharibi, alitaja mkusanyiko wa maneno muhimu ya kifalsafa na kielimu, akisema: Uhusiano wa kimaarifa, mada katika ontolojia na antropolojia, ubinadamu (humanism), uhuru wa mtu binafsi, asili ya starehe na manufaa, pragmatism, tafsiri za usiabo za maandiko, liberalism, sekularism na nadharia ya “mwisho wa historia” ni miongoni mwa misingi ya ustaarabu huu, ambayo imepenya katika sayansi za kijamii, mfumo wa malezi, sanaa, mtindo wa maisha na miundo ya kijamii.
Aliongeza kuwa: Kunufaika na mafanikio ya kisayansi ya Magharibi ni jambo la kiakili, lakini kupuuza programu ya kifalsafa inayotawala mafanikio hayo ni kosa; na wanahawza, hasa wale wa elimu na wasomi, wanapaswa kuingia katika uwanja huu kwa maarifa ya kina na mtazamo wa uchambuzi.
Kukitambua kizazi kipya; sharti la mafanikio katika tablighi
Mkuu wa hawza za elimu ya dini, huku akisisitiza tofauti za kizazi cha leo na vizazi vilivyopita, alisema: Kijana wa leo anakabiliwa na wingi mkubwa, wa aina mbalimbali na wa kasi wa taarifa, na anakutana na hali kama kukosa subira, kuchanganyikiwa, kuchelewa kukubali ukweli wa kiroho na mazingira ya udanganyifu; hivyo, kuelewa saikolojia ya kizazi kipya ni muhimu kwa mafanikio ya tablighi.
Mjumbe wa Baraza Kuu la Hawza alisema: Kijana muumini wa leo yuko katika mazingira magumu zaidi kuliko zamani, na thamani ya ustahimilivu wake ni kubwa zaidi; vivyo hivyo, thamani ya kazi ya mubalighi na mlezi pia huongezeka katika hali hizi.
Kufafanua upya tablighi; kutoka kuwasilisha ujumbe hadi malezi endelevu
Ayatollah A‘rafi, alisisitiza umuhimu wa kurejea katika maana ya kina ya Qur’ani ya tablighi, akisema: Tablighi haipaswi kuishia katika kuhamisha taarifa, bali inapaswa kuwa mchakato wa malezi, utafiti na athari ya kina katika nafsi ya hadhira.
Alibainisha kuwa, sekta ya elimu na malezi ina nafasi muhimu katika njia hii, na akasema: Taasisi zote zinapaswa kujiona zina deni kwa elimu na malezi na kuwasilisha mipango ya utekelezaji wa hati ya mageuzi ya elimu.
Mkuu wa hawza za elimu ya dini pia alisisitiza umuhimu wa kuboresha maisha ya walimu na wasimamizi, akisema: Bila kuzingatia hali ya maisha, haiwezekani kufikia malengo makubwa ya malezi.
Mapinduzi ya Kiislamu na kuondolewa kwa mfumo wa kifalme
Mjumbe wa Baraza Kuu la Hawza huku akirejelea mafanikio ya Mapinduzi ya Kiislamu alisema; kuondolewa kwa mfumo wa kifalme ni miongoni mwa mabadiliko muhimu katika historia ya kisasa ya Iran. Alisema Mapinduzi ya Kiislamu yaliuangusha mfumo usio na mantiki ya uhalali uliokuwa umejengwa juu ya nguvu, na yakarejesha uhuru wa nchi.
Alisisitiza umuhimu wa kusoma upya historia ya kisasa kwa ushahidi kwa ajili ya kizazi cha vijana, na akataka kutayarishwa maudhui sahihi, yenye ushahidi na yanayolingana na lugha ya kisasa ili kufafanua mafanikio ya Mapinduzi.
Mwisho, Ayatollah A‘rafi aliwashukuru wasimamizi na wanaharakati wa taasisi za hawza, na kusisitiza kuendeleza uratibu na juhudi za pamoja za kuimarisha uwanja wa kitamaduni na tablighi katika kuelekea mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Maoni yako